Sunday 26 July 2015

Hifadhi ya Taifa ya Serengeti Eden ya Afrika

    HIFADHI ya Taifa ya Serengeti inayopita katika mikoa ya Arusha,Mwanza,Mara na Shinyanga ni eneo pekee duniani lenye kundi kubwa la wanyama wanaohama katika mfumo mzima wa mlishano.
   Inasemekena neno Serengeti linatokana na neno la kimasai la sirenget lenye maana ya  uwanda mpana wa nyasi fupi,malisho mengi na maji ya kutosha pengine ndiyo maana hifadhi hiyo inapewa majina mengi kama vile bustani ya Afrika na Edeni ya Afrika kutokana na utajiri wa maliasili uliopo ndani ya hifadhi hii.
Hifadhi ya Taifa ya Serengeti yenye ukubwa wa  kilometa za mraba 14,763 ilianzishwa mwaka 1951, ni Hifadhi ya Taifa ya pili kwa ukubwa nchini ikitanguliwa na hifadhi ya Taifa ya Ruaha yenye ukubwa wa kilometa za mraba 20,226.
     Umaarufu wa hifadhi ya Taifa ya Serengeti  unatokana na kuwa na misururu mirefu ya nyumbu wanaohama kwa makundi  na kuvuka hata mpaka wa Tanzania hadi hifadhi ya wanyama pori ya Maasai Mara nchini Kenya ambapo takwimu za TANAPA zinaonyesha kuwa kila mwaka zaidi ya nyumbu milioni moja,pundamilia 200,000, swala tomi zaidi ya 300,000 na pofu 12,000 huunga misafara ya kutafuta malisho na maji 
Hifadhi ya Taifa ya Serengeti huchukuliwa kama moja ya maajabu ya dunia kutokana na tendo la uhamaji wa nyumbu kutoka kusini hadi kaskazini na kurudi, tendo ambalo linafanyika mara moja tu kwa mwaka tendo hilo linaifanya hifadhi hii kuwa Eden ya Afrika na kupendwa kutembelewa na watu wengi ulimwenguni kote. Licha ya nyumbu wanyama wengine maarufu walao nyama katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti ni chui na samba, ambapo utafiti umebaini kuwa ukubwa wa hifadhi hii umesaidia kudumisha uhai wa wanyama waliokuwa katika hatari ya kutoweka kama vile faru weusi na duma
       Watalii wanaotembelea Hifadhi ya Taifa ya Serengeti  kutokana na makundi makubwa ya nyumbu wameifanya hifadhi hiyo kuwa maarufu Afrika mashariki na ulimwenguni kote hali iliyosababisha shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu na Sayansi UNESCO  kuitangaza Serengeti kuwa  eneo la urithi wa Dunia  kwa kuwa ndiyo eneo pekee ulimwenguni lililosalia kundi kubwa la wanyama wahamao.  Hifadhi ya Taifa ya Serengeti ipo umbali wa kilometa 335 kutoka Arusha ikiambaa kaskazini katika mpaka na nchi ya Kenya,kwa upande wa magharibi inapakana na na ziwa Viktoria.
      Hifadhi hii inafikika kwa kukodi ndege kutokea jijini Dar es salaam,Mwanza,Kilimanjaro na Arusha pia kwa barabara kutokea Arusha,Musoma na Mwanza,wakati mzuri wa kutembelea hifadhi hii ili kuona uhamaji wa nyumbu ni kuanzia mwezi Desemba hadi Julai.
   ADVERTISE WITH US: +2250653683428
    Email: teresiamsanga@gmail.com

No comments: